Monday, August 27, 2012

Bw Fadhil Ngajilo katika moja kati ya mikutano yake akiwa mwenyekiti UVCCM mkoa wa Iringa
Ndg. Fadhili Fabian Ngajilo alikuwa akiwasilisha ripoti ya kuboresha muundo wa UVCCM mwezi Juni, 2012 ndani ya ukumbi wa NEC-CCM katika jengo la White House Makao Makuu ya CCM, Dodoma.
YAH:
NDG. FADHILI FABIAN NGAJILO
KUGOMBEA NAFASI YA MWENYEKITI WA CCM MKOA WA IRINGA
Kutokana na uchaguzi unaoendelea ndani ya Chama cha Mapinduzi, Mimi Fadhili Fabian Ngajilo (pichani) ambaye ni Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Iringa nitakayestaafu mwezi wa Oktoba kutokana na umri wangu kuvuka ukomo wa kikanuni wa miaka 30, sasa ninagombea nafasi ya Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa, nimechukua fomu tarehe 26 Julai 2011. Ninagombea nafasi hii kwa kuwa nimejipima, nimejichunguza na kuona kuwa nafasi hiyo ninaimudu. Ninauzoefu na shughuli za chama kupitia idara nilizoziongoza kama Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM), Ujumbe wa Kamati ya Siasa ya CCM Mkoa na Halmashauri Kuu ya CCM ya Mkoa wa Iringa, Mjumbe Mkutano Mkuu wa CCM Taifa na Baraza Kuu la Taifa la Umoja wa Vijana wa CCM. Lakini pia ukitazama Wasifu wangu utagundua kuwa mimi nimeanzia ngazi ya chini (mtaa) kuwa kiongozi, nimepanda taratibu hadi mkoani. Nina malengo kadhaa endapo nitafanikiwa kuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa, mimi ninaamini kuwa ‘Fikra sahihi na uchumi bora wa chama utaifanya CCM kuwa imara zaidi na kuendelea kushika dola’ kwa hiyo hii ndio itakuwa kauli mbiu itakayoongoza chama mkoa wa Iringa kwa kipindi cha miaka mitano ijayo, malengo mengine ni;
1. Kama nilivyoonyesha awali kuwa lengo kuu la kuwania nafasi hii ni kuujenga uchumi wa chama katika ngazi za kata na matawi ya chama. Tutaanzisha kampuni ya kibiashara itakayoendeshwa na wataalamu na itajikita katika kubuni, kuanzisha na kusimamia miradi mbalimbali ambayo itamilikiwa na kata na matawi yote ya CCM Mkoa wa Iringa. Tutatoa kipaumbele kwenye miradi ya Kilimo, Misitu, Majengo na Usafirishaji.
2. Nitasimamia mshikamano wa wanachama na viongozi wa CCM Mkoa wa Iringa. Njia kuu ya kutekeleza hili ni kwa kutenda haki kupitia vikao vya maadili vya chama vya ngazi zote. Kwa hiyo tutahimiza ngazi zote kufanya vikao vingi kwani ndio nguzo muhimu ya uimara wa chama.
3. Nitahakikisha Chama cha Mapinduzi (CCM) kinaendelea kushika dola, hakuna jimbo la uchaguzi litakaloenda upinzani chini ya uongozi wangu. Njia ya kufanikisha hili ni kwa kuisimamia Serikali kupitia Halmashauri za Wilaya katika kutekeleza ilani ya uchaguzi ya CCM. Nitaongeza nguvu kwenye kuziba mianya ya ufisadi dhidi ya mali za umma katika Halmashauri zetu na kuhakikisha fedha zinazotengwa kwa kazi za maendeleo inafanya hivyo.
4. Nitaimarisha idara za Itikadi na Uenezi, Fedha na Uchumi, Umoja wa Wanawake (UWT), Umoja wa Vijana (UVCCM) na Jumuiya ya Wazazi mkoa wa Iringa. Vyombo hivi vitaimarishwa kwa kupewa watendaji wenye weledi, vifaa na kuimarisha uchumi kupitia miradi yake. Makambi ya kuwaandaa makada kiitikadi na kisiasa yatafanyika kupitia programu maalumu itakayoanzishwa na kusimamiwa katika Chuo cha Ihemi, mpango huu utaitwa ‘CCM Vital Program’ kwa kifupi CCMVP. Mpango huu utaandaa makada wakufunzi, Utaanzisha madarasa ya Itikadi ngazi za Matawi na Kata, utaandaa vitabu na vijarida vya kujisomea masuala mbalimbali ya chama.
5. Tutawaenzi wazee kwa kuwaanzishia Umoja wao (Umoja wa Wazee wa Chama cha Mapinduzi) utakaokuwa na jukumu la kutoa ushauri kwa chama, tutaanzisha Umoja huu katika ngazi za wilaya zote za mkoa wa Iringa. Wazee watakuwa wakikutana katika mabaraza yao kila mara, wataanzisha shughuli za michezo na jadi za wazee, ujasiriamali nakadhalika.
6. Nitaamsha ari mpya kwa wanachama wa CCM Mkoa wa Iringa ili wajisikie na kujivunia uimara wa chama chao. Tutafanya hivyo kwa kusimamia maamuzi na fikra sahihi na za kisasa ndani ya chama. Tutafanya mikutano ya kuhamasisha maendeleo, na kujibu hoja na propaganda chafu za upinzani dhidi ya CCM.
7. CCM Mkoa wa Iringa itajishughulisha na shughuli za kijamii wakati wa uongozi wangu ikiwamo Michezo kwa vijana, maveterani, wanawake na wazee. Kundi la vijana litapewa kipaumbele katika kuhamasisha utengenezaji wa fursa za ajira. Lakini pia Mkoa utajishughulisha na kuhamasisha shughuli za ujasiriamali na biashara katika sekta zote.
WASIFU WANGU(CV)
(a) KUZALIWA NA KAZI
Mimi ni kijana niliyezaliwa tarehe 27 Juni, 1979 Manispaa ya Iringa. Kwa sasa mimi ni Mhadhiri Chuo Kikuu cha St. John’s University. Lakini pia nimeshawahi kuwa Mwendeshaji wa Semina (Seminar Leader) katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam.
(b)ELIMU NA MAFUNZO YA SIASA
Nimesoma Shule ya Msingi ya Mapinduzi na Chemchem zote zikiwa Manispaa ya Iringa, Baadae mwaka 1995 nilijiunga Shule ya Sekondari ya Lugalo ya Manispaa ya Iringa kwa ajili ya kidato cha I-IV, na mwaka 1999 nilijiunga na Shule ya Sekondari ya Makongo JWTZ iliyopo Dar es Salaam kwa ajili ya kidato cha V na VI. Kati ya mwaka 2003-2006 nilisoma Shahada ya Historia na Mambo ya Kale (B.A. History and Archaeology) ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam, mwaka 2006 nilichaguliwa kusoma Shahada ya Historia katika fani za Siasa na uchumi (M.A History) katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Kwa sasa naandika andiko linalohusu ajira za watoto kwa ajili ya Shahada ya Udaktari wa Falsafa (Ph.D). Pia mimi ni mtaalamu wa masuala ya kompyuta mwenye cheti cha Computer Literacy Certificate kutoka Chuo cha Compware College. Pamoja na yote hapo juu nimefanya tafiti mbalimbali za kitaaluma.
Nimehudhuria mafunzo na kambi mbalimbali za siasa zikiwemo zilizoandaliwa na Taasisi ya Ujerumani ya Friedrich Ebert Stiftung (FES) mwaka 2009. Pia Mimi ni mkufunzi wa Siasa na Itikadi kupitia mafunzo (TOT) ambayo niliyapata mwaka 2010 chini ya Mzee Kingunge Ngombalemwiru.
(c) UZOEFU KATIKA UONGOZI
§ Kwa sasa ni Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Iringa, ambaye ninastaafu mwezi wa Oktoba mwaka 2012.
§ Pia mimi ni Mwenyekiti wa Wenyeviti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Tanzania, ambaye pia ninastaafu nafasi hiyo mwezi Oktoba.
§ Nilikuwa Mjumbe wa Kamati Maalumu ya Baraza Kuu la UVCCM Taifa ya kuboresha Muundo na Madhumuni ya Umoja huo, kamati ambayo imezunguka nchi nzima kukusanya maoni ya wanachama.
§ Mwaka 2010 niliwania nafasi ya kugombea Ubunge kupitia kura za maoni katika Jimbo la Iringa Mjini. Lakini kura hazikutosha.
§ Kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita nimekuwa Mjumbe wa Kamati ya Siasa na Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Iringa.
§ Kabla ya mwaka 2008 nilitumikia chama kwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Vijana wa Chama cha Mapinduzi Manispaa ya Iringa. Nilikaimu uenyekiti wa UVCCM wa kata ya Kwakilosa, Manispaa ya Iringa, ambako pia nilikuwa Meneja kampeni wa kata uchaguzi mkuu wa mwaka 2005.
§ Nilikuwa Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Jangwani, Kata ya Kwakilosa, Manispaa ya Iringa kati ya mwaka 2009 hadi 2004. Hii inaonyesha kuwa nimeanza uongozi kuanzia ngazi ya chini kabisa.
§ Nikiwa nasoma Chuo Kikuu cha Dar es salaam, nilikuwa Mwenyekiti wa Wanafunzi kupitia taasisi ya ‘Iringa University Students Association’ (IRUSA)
§ Lakini pia nilipokuwa nasoma Shule ya Sekondari ya Makongo High School nilikuwa Mwenyekiti wa wanafunzi kupitia umoja wao uitwao ‘Tanzania Youth Catholic Student’s Society (TYCS)’
Kauli Mbiu yangu
‘Fikra sahihi na uchumi bora wa chama utaifanya CCM kuwa imara zaidi
na kuendelea kushika dola’
Kidumu Chama Cha Mapinduzi!
SIMU YANGU: 0767-609477

No comments:

Post a Comment